Thursday, August 14, 2014

FISI MWENYE KICHAA AVAMIA MAKAZI YA WATU NA KUJERUHI


MATUKIO yanayohusishwa na imani za kishirikina ya watu kujeruhiwa,kuuawa na fisi na kisha kugombea nyama yake na kwenda kuipika kwa ajili ya kitoweo yamezidi kushika kasi kwenye mkoa huu wa Geita.

Juzi,Fisi mwingine mwenye kichaa amevamia makazi ya watu na kung’ata watu watano sehemu mbalimbali ya miili yao wilayani Bukombe mkoani Geita.

Mganga mkuu wa hospitali ya Wilaya ya Bukombe Dk Tenesigwa amethibitisha kupokea kwa majeruhi hao kutoka Kijiji cha Ililika Wilayani humo.

Amewataja majeruhi hao kuwa ni Hamis Mpendakula,Mateso Manyanda Bugolo,Manyanda Bugolo,Dalali Selemani,na Mhoja Deusi.

Amefafanua kuwa kati ya hao,Hamis Mpendakula amejeruhiwa vibaya sana na kufunuliwa ngozi ya kichwa pamoja na uso na kufanya fuvu la kichwa kubaki wazi na fuvu hilo limepasuka.

Amesema wengine wamevunjwa vunjwa vidole vyao na kujeruhiwa baadhi ya viungo vya miili yao na wamewapa rufaa ya kwenda hospitali ya Bugando kwa matibabu zaidi.

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ,mkuu wa Wilaya ya Bukombe Amani Mwenegoha ametoa wito kwa wananchi wa Wilaya hiyo kuchukua hatua ya kujihadhari na kuimarisha ulinzi wa Jadi(sungusungu).

Mwenegoha amesisitiza kuwa,kuanzia sasa kila Kijiji kwenye Wilaya yake kinatakiwa kuimarisha ulinzi wa jadi na  kwa kuwa fisi aliyefanya kitendo hicho ametajwa kuwa na kichaa aliwataka wananchi kuacha kutembea hovyo hasa nyakati za usiku hadi hapo fisi huyo atakapopatikana na kuuawa.

‘’Nina imani huyu Fisi atapatikana haraka ipasavyo na ninawaomba wananchi iwapo watasikia kelele kwenye mazizi yao ya ng’ombe nyakati za usiku wajue ndiye fisi huyo na wapige mayowe ili watu wengi wakusanyike na kumzingira hadi kumuua’’alisema Mwenegoha.

Mkuu wa wilaya huyo tayari amewaagiza maafisa wa wanyamapori kwenye Wilaya yake kufanya msako usiku na mchana hadi hapo watakapohakikisha fisi huyo ameuawa kwa kuwa anatishia uhai wa watu wa Wilaya hiyo na maeneo ya jirani.

Mwishoni mwa wiki iliyopita baadhi ya wakazi wa kijiji cha Ihayabuyaga,kata ya kalangalala Wilayani Geita waliamua kugawana nyama ya fisi  aliyegongwa na gari usiku katika barabara kuu ya Mwanza Kagera wakati akikatiza mitaa ya mji huo jirani na ilipo gereji ya mabasi ya Lushanga.

Mbali na hilo,matukio haya yamekuwa yakitokea kwa wingi wilayani Geita yakiwemo ya watu kushambuliwa na mnyama huyo aina ya fisi hususani watoto chini ya Umri wa miaka Mitano na hivi karibuni fisi mwingine alivamia mtaa na kuanza kushambulia watu hovyo kwa kuwauma kabla ya polisi kufika eneo hilo na kumuua kwa risasi kisha kutoa mwanya kwa wananchi kugombea nyama yake na kuifanya kitoweo.

Tukio hilo la kusitaajabisha na ambalo liliacha maswali mengi,lilitokea mwishoni mwa mwezi Juni,majira ya saa 9 alasiri katika mtaa wa Kabahelele,Kata ya Katoro Wilaya ya Geita Mkoani Geita.
Wakati polisi wanafika eneo hilo,tayari Fisi huyo alikuwa amefanya madhara kwa watu watatu ambao waling’atwa sehemu za miguuni na midomoni hali iliyowalazimu polisi kutawanya watu kisha walifanikiwa kumuua fisi huyo kwa kumpiga risasi zaidi ya mbili.
Waliojeruhiwa na Fisi katika tukio hilo,walikuwa ni Bugamba Zumbe(21),Peter Francis (32),na mwingine ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja wote wakazi wa mtaa huo wa Kabahelele.
Baada ya Fisi huyo kuuawa,baadhi ya wananchi wa eneo hilo nusura wauane kwa kukatana visu wakigombea nyama ya mnyama huyo na walipohojiwa na Malunde1 blog kuhusu nini sababu za kugombea nyama hiyo walidai inaliwa na kwamba ikipikwa vizuri inazidi hata ile ya ng’ombe.
Tukio jingine ni la Masumbuko John(35) mkazi wa Nyabulanda Tarafa ya Nyang’hwale Wilayani Nyang’hwale Mkoani Geita aliyeuawa kwa kushambuliwa na Fisi na kuliwa,sehemu za Tumbo,mguu mmoja ukiwa umebaki mfupa na ule wa kulia  pamoja sehemu za usoni kichwani na kifuani.
Ofisa Misitu na Maliasili wa Wilaya ya Geita Kasika Gamba amedai chanzo cha Fisi kushambulia watu,na kuonekana sehemu za mjini ni kutokana na uharibifu wa mazingira katika Hifadhi za Mistu hali ambayo imesababisha wanyama hao kuzagaa kwenye makazi ya watu kutokana na kukosa sehemu ya kijihifadhi na kujipatia chakula.
 Daktari wa Mifugo wa Wilaya ya Geita Thobias Kiputa, amewataka wananchi kuepuka kula hovyo nyama za wanyama ambao siyo wanyama(Meat Animals)ambao ni wala nyama kama Fisi ambao hawajakaguliwa kwa alichodai kula nyama ya wanyama wala nyama kama fisi,ambao hawajakaguliwa wanaweza kuwa na magonjwa mbalimbali yanayoweza kuwasababishia madhara ya afya.

Na Victor Bariety-Malunde1 blog-Geita

No comments:

Post a Comment