Monday, September 29, 2014

KADA WA CHADEMA ALIYEWAHI KUGOMBEA UBUNGE AJIUNGA CCM


Aliyewahi  kugombea ubunge wa Mlalo Wilaya ya Lushoto mkoani Tanga kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) mwaka 2005, Charles Kagonji amekihama chama hicho na kurejea katika Chama Cha Mapinduzi (CCM).
 
Kagonji alirejea CCM katika mkutano wa hadhara, uliofanyika Sunga Kata ya Sunga Tarafa ya Mtae wilayani Lushoto, jana, mbele ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana.
 
Kagonji amekaa katika chama hicho kikubwa cha upinzani kwa miaka minne, kabla ya kuamua kukihama jana.
 
Kabla ya kujiunga na Chadema, Kagonji ambaye kitaaluma ni Mwandishi wa Habari, aliwahi kuwa Mbunge wa Jimbo hilo la Mlalo kwa miaka 15 kutoka mwaka 1990 hadi mwaka 2005 kwa tiketi ya CCM.
 
Kabla ya kuwa mbunge, Kagonji ambaye alikuwa mpigapicha maarufu na mwandishi wa habari mwandamizi, alifanya kazi kwa miaka mingi katika Idara ya Habari (Maelezo).
 
Akihojiwa kwa njia ya simu jana sababu zilizomfanya ahame Chadema, alisema kuwa ameamua kurudi nyumbani (CCM), kwa sababu ndiyo iliyomlea na anafahamu vizuri historia, mila na desturi zake.
 
Alisema Chadema hajui mila na desturi zake, lakini ni chama kizuri na chenye nguvu, bali yeye ameamua kurejea nyumbani. Kagonji alisema alipokuwa Mbunge wa Mlalo, alijitahidi kufanya mambo mengi makubwa ya maendeleo kwa kushirikiana na wananchi.
 
Kwa mfano, alisema akishirikiana na wananchi, walijitahidi kuanzisha shule za sekondari za kata na hadi anaondoka mwaka 2010, jimbo hilo lilikuwa na sekondari 10. Kwa sasa sekondari zimeongezeka hadi zaidi ya 16.
 
“Pia kwa kushirikiana na Serikali na wananchi tumeweza kujenga barabara na miundombinu ya huduma za maji. Huduma za umeme na simu pia zimeboreshwa kwa kiwango kikubwa,” alisema.

No comments:

Post a Comment