Saturday, May 31, 2014

KIJANA AZUA BALAA KIJIJINI BAADA YA KUSADIKIWA KUWA NI MSUKULE ,MAMIA YA WANANCHI WAFULIKA KUSHUHUDIA .JIONEEE TUKIO ZIMA HAPA.



Mkuu wa kituo cha polisi wilaya ya Kishapu Samwel Kijenga akizungumza na wananchi wa kijiji cha Ilebelebe kata ya Itilima wilayani humo,mara baada ya kuvunja nyumba iliyokuwa ikisadikiwa kuwa ina misukule ndani na kukuta hakuna mtu ambapo aliwataka wananchi kuendelea na shughuli zao za maendeleo waachane na imani hizo potofu.


Huyu ndiyo kijana anayesadikiwa kuwa aliwekwa msukule kwenye nyumba ya ajuza ambayo ilikuwa haitumiki na anadai alikuwa na wenzake watatu lakini baada ya polisi kuvunja nyumba hiyo hawakuona watu .

Nyumba inayosadikiwa kuwa inamisukule ambayo ilikuwa imefugwa na ajuza Nyanzila Mbasu(65) katika kijiji cha Ilebelebe wilaya ya Kishapu,Shinyanga.
Pata habari zaidi hapa.

MAMIA ya wananchi wa kijiji cha Ilebelebe kata ya Itilima wilaya ya Kishapu mkoa wa Shinyanga  wamefurika  kushuhudia tukio la kijana mmoja anayesadikiwa kuwa ni msukule,  ambaye alionekana jirani na nyumba ya kikongwe mmoja aliyefariki dunia  mei 26 mwaka huu kwa kukatwakatwa mapanga  kwa tuhuma za ushirikina na kudai kuwa alikuwa anahifadhiwa na ajuza huyo.



Tukio hilo limetokea ikiwa ni siku moja baada ya Ajuza  aliyejulikana kwa jina la Nyanzala Mbasu (65) kuvamiwa na watu wasiojulikana na kumcharanga mapanga  nyumbani kwake kisha kutokomea kusikojulikana ,ambapo siku ya mazishi yake yaliyofanyika juzi ndipo kijana huyo alikutwa na wanachi nyuma ya nyumba hiyo saa tatu usiku akizunguka na kusema kaamua kutoka nje baada ya kukosa chakula.

Kijana huyo anayesadikiwa kuwa ni msukule anajulikana kwa jina la Ndaki Samola ambaye alidai anatoka kijiji cha Ubale kata ya Samuye wilaya ya Shinyanga,huku akizungumza kwa shida alisema alifika kijijini humo kwa ajili ya kuoa, bila ya kufafanua ni kipindi gani amekaa na kwamba alikuwa akiishi kwenye nyumba ya bati ya ajuza huyo na wenzake wawili.

Mwenyekiti wa kijiji hicho cha Ilebelebe Thomas Nkindo alisema tukio hilo limewashangaza kwani kijana huyo hajawahi kuonekana kijijini humo hata siku moja ,hali ambayo imewapa wasiwasi wananchi kutokana na maneno aliyoeleza kwamba alikuwa kwenye nyumba ya ajuza huyo ambayo imefungwa kwa muda mrefu na haitumiki.
Alisema baada ya kumuhoji sungusungu alidai kuwa kilichomtoa ndani ni  njaa na kwamba kawaancha wenzake wawili mmoja akiwa ni mwanamke ambao walikuwa wanakaa pamoja nayeye, alikuja kwa ajili ya kuoa na kufikishiwa kwenye nyumba hiyo ya tope ambayo imeezekwa kwa bati iliyokuwa ikimilikiwa na marehemu.

Afisa mtendaji wa kijiji hicho Emmanuel  Asili alisema marehemu Mbasu kabla ya kufikwa na mauti siku hiyo ya tukio asubuhi alikuwa amealika wanawake, ambao walifanya kazi ya kumsaidia kukata mapalage ya viazi (maarufu kama michembe) ndipo usiku huo huo alivamiwa na kuuawa majira ya saa 1.30  wakati akimpatia mbwa wake chakula.

“Kilichotushitua zaidi huyo kijana Ndaki alikuwa anuka harufu ya nyama wakati tunamuona na ukizingatia mchana kwenye mji huo ulipokuwa msiba walikuwa wamechinja mbuzi,moja kwa moja wananchi walimtilia mashaka inawezekana akawa ni msukule kwa kulinganisha na maelezo yake “alisema Asili.

Kutokana na mashaka hayo waliamua kutoa taarifa kwa jeshi la polisi huku kijana huyo akiwa amehifadhiwa kwa muda katika ofisi ya afisa mtendaji wa kijiji kwa uangalizi zaidi,mara baada ya askari kufika eneo la tukio walizungumza na wananchi na kuamuru mlango wa nyumba hiyo uvunjwe ili kuona kilichomo ndani na kuiondoa wasiwasi  jamii ambapo walikuta bati lililochakaa,beseni na ndoo.

Akizungumza na wananchi mkuu wa kituo cha polisi wilaya ya Kishapu ASP Samwel Kijenga aliwataka kutoa ushirikiano ili kuwabaini watu waliosababisha mauaji hayo ya kinyama,ambapo alisema wataendelea kufanya upelelezi na kwamba waondowe wasiwasi nyumba waliyokuwa wakihofia wameangalia hakuna kitu hivyo waendelee na shughuli za maendeleo.

Hata hivyo wakati kijana huyo akiwa tayari amepandishwa ndani ya gari la polisi kwa ajili ya kupelekwa kufanyiwa uchunguzi kama anamatatizo ya akili,alitokea baba mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Nyalali Chaba na kudadi kuwa anamfahamu ni mdogo wake anasumbuliwa na tatizo la akili .

Kamanda wa jeshi la polisi mkoani Shinyanga Evarist Mangalla amethibitisha kutokea kwa tukio hilo la mauaji ya ajuza wa miaka (65) na tayari  watu wanne wanashikiliwa kwa ajili ya mahojiano zaidi wakati wakiendelea na upelelezi.

 





No comments:

Post a Comment