Wednesday, May 14, 2014

MIFUKO YA HIFADHI YA JAMII YATAHADHARISHWA KUACHA KUFANYA KAZI KWA UTAPELI


MIFUKO ya hifadhi ya jamii nchini imetahadharishwa kuacha kufanya kazi kwa kutapeli watumishi wapya wa serikali hususani waajiriwa wapya kwa kutoa fomu ambazo zimeshajazwa bila kutoa ushauri  mzuri, hali ambayo inasababisha baada ya muda wateja wao kujutia kujiunga na mifuko hiyo.

 Kauli hiyo ilitolewa jana na mkuu wa wilaya ya Shinyanga Annarose Nyamubi kwenye semina ya elimu juu ya hifadhi ya jamii kwa viongozi wa serikali mkoa wa Shinyanga,ambapo alisema baadhi ya mifuko haifanyi kazi zake kwa uwazi  hivyo kuwatapeli watumishi hasa waajiriwa wapya ambao wanakuwa hawaifahamu vizuri.

Mkuu wa wilaya aliitaka mifuko hiyo kufanyakazi zake kwa uwazi na kutoa huduma iliyobora kwa wateja wao ili kuwahamasha watumishi wengine kutoka serikalini,mashirika,taasisi na watu binafsi kujiunga ili kujiwekea akiba ya uzeeni pamoja na mafao mengine ukiwemo uzazi na matibabu .

“ Inaumiza pale ambapo unawekeza baada ya miaka mitano halafu kinafanana na mtu aliyewekeza leo wakati gharama za maisha zinapanda kila kukicha,ninawaomba ndugu zangu mnaosimamia mifuko hii kwenda na mabadiliko ya hali halisi iliyopo”alisema Nyamubi.

Nyamubi alisema mfuko wa hifadhi ya jamii(NSSF) umekuwa ukilalamikiwa na watumishi wengi kwa kushindwa kuboresha huduma zake, hali hiyo inaweza kusababisha kukosa wananchama na malengo yao kutofikiwa na kutolea mfano wakati wa mei mosi mabango mengi yalikuwa yakiulenga mfuko huo kwa kuumiza watumishi katika mafao.

Semina hiyo ya siku moja iliandaliwa na mamlaka ya usimamizi wa sekta ya hifadhi ya jamii (SSRA)alisema mifuko hiyo  inatija kubwa iwapo jamii itaitumia vizuri katika kujiletea maendeleo na kuweka akiba ya uzeeni,ambapo yote hayo yatafanikiwa kwa kufanyakazi kwa uwazi na kuboresha huduma wanazozitoa .

Kwa upande wake mwezeshaji wa semina hiyo kutoka (SSRA) Dar es salaam Mohamed Nyasama,alisema mpaka sasa ni 4.5 ya watanzania wote ndiyo wamejiunga na mifuko ya hifadhi ya jamii,idadi ambayo bado iko chini na kuwataka watanzania kubadilika na kuwekeza kupitia mifuko ya hifadhi ya jamii kwa kuwa ni mkombozi wa kweli.

Alisema mamlaka hiyo inafanya kazi ya kutetea na kulinda maslahi ya wanachama,wafanyakazi na wastaafu ili kuleta faida kwa wateja kwa kuboresha uhakika wa maisha yao ya baadaye,kinga dhidi ya majanga kwa watanzania na kukuza uwekezaji nchini.

Naye katibu tawala wilaya ya Shinyanga Boniphace Chambi alisema utendaji mbovu wa baadhi ya mifuko unakatisha tamaa  watumishi kujiunga na mifuko yao, kutokana na kuona hali halisi jinsi wazee wastaafu wanavyohangaika kufuatilia mafao yao wakati takwimu zote zipo lakini kwenye malipo inakuwa tatizo.

Mwenyekiti wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi mkoa wa Shinyanga (TUCTA)Fue Mlindoko,alisema kero kubwa wanazokumbana nazo ni mafao kutokuwa sawa miongoni mwa watumishi wakati wakitambua fika tarehe za kuajiriwa na kustaafu, lakini cha kusikitisha wakati wa kuchukuwa mafao yanakuwa kidogo kinyume na matarajio yao.

No comments:

Post a Comment