Thursday, August 14, 2014

MTU NA MPENZI WAKE WAKUTWA NA MAITI YA KIKONGWE HOTELINI IKIWA KWENYE MFUKO WA KUSAFIRIA.

Tommy Schaffer, mwenye umri wa miaka 21,amekamatwa pamoja na mpenzi wake Heather Mack.
Polisi wa kisiwa cha Bali nchini Indonesia wanawashikilia watu wawili baada ya mwili wa mwanamke wa kimarekani kuonekana kwenye mfuko wa kusafiria.
Binti wa mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 19 pamoja na mpenzi wake mwenye miaka 21 wameshikiliwa na polisi katika hoteli iliyopo ufukweni siku ya Jumatano.
Marehemu mwenye umri wa miaka 62 Sheila Wiese Mack, alipatikana katika buti ya taksi akiwa ndani ya mfuko wa kusafiria katika hoteli.
Afisa wa Indonesia amesema marehemu huyo ameonekana kuwa na majeraha katika uso na kichwani mwake.
"Kulikuwa na ishara ya mahangaiko kwa muathirika huyo kutokana na kuwa na michubuko katika mikono na vidole vyake vikiwa vimevunjwa,’’shirika la habari la reuters lilimnukuu Afisa Ida Bagus Putu Alit, akisema
Polisi waliwakamata wapenzi hao baada ya kuwakuta katika hoteli tofauti huko Bali.
Mkuu wa polisi katika mji mkuu wa Bali wa Denspasar, Djoko Hari Utomo, amewaambia waandishi wa habari kuwa wapenzi hao ambao ni watuhumiwa walikodi teksi na kuweka mfuko wa kusafiria kwenye buti.
Dereva wa teksi hiyo alisema walimwambia wanakwenda kuangalia hoteli lakini watarudi.
Ripoti inasema dereva wa teksi alishuku mfuko huo ambao ulikuwa na damu ndani yake, na kuwaomba polisi kuufungua.
Mkuu wa polisi alisema baada ya mwili kugundulika, polisi waliwapata wapenzi hao wakiishi katika hoteli nyingine huko Bali.
Polisi walisema uchunguzi wa mwili wa Bibi Von Wiese-Mack unaendelea.
Taarifa ya ubalozi wa Marekani nchini Indonesia inasema ubalozi huo umepata taarifa za kifo cha raia wa Marekani na kwamba watu wawili wamekamatwa kuhusiana na tukio hilo.
Mama na binti yake wameripotiwa kuwa wanaishi Chicago, Marekani.
  Via :bbc swahili

No comments:

Post a Comment