Friday, September 5, 2014

MWALIMU MMOJA AFUNDISHA ZAIDI YA WANAFUNZI 300 HUKU WATOTO WAKIJISAIDIA VICHAKANI KUTOKANA NA KUWA NA CHOO KIMOJA TU

Mwalimu Laiton akiwa akiwafundisha wanafunzi wake waliochanganyika madarasa kutokana na uhaba wa madarasa

Baadhi ya watoto wa shule ya msingi Ishungu wakiwa katika picha ya pamoja na mwalimu wao

Mwalimu Laiton akiwa na wanafunzi wake muda wa mapumziko


Watoto wakiwa darasani



Choo hiki hutumika na zaidi ya watoto 300 wa jinsi zote


Baadhi ya wazazi na viongozi wa kijiji
Wananchi wa Kijiji cha Maendeleo Kata ya Ruiwa wameiomba Serikali kuingilia kati hatma ya shule ya Msingi ya Kijiji hicho kutokana na uhaba wa walimu na madarasa ya kusomea.
Wakionge na Mbeya yetu kwa masikitiko baadhi ya wazazi walisema uongozi wa Kijiji hicho umeshindwa kuiendeleza shule hiyo licha ya kukusanya fedha kutoka kwa wananchi na wafugaji Kijijini hapo.
Jason Halinga mmoja wa wazee maarufu Kijijini hapo alisema kuwa yeye ana watoto sita wanaosoma shuleni hapo wanaosoma darasa la kwanza hadi la sita wakifundishwa na Mwalimu mmoja tu aliyefahamika kwa jina la Laiton Ngoli.
Mwalimu huyo aliyeanza kufundisha mwaka 2007 hajawahi kulipwa mshahara wowote licha ya kufundisha kila siku ingawa wazazi wamekuwa wakijitahidi kuchangia shilingi elfu moja kwa kila mwanafunzi lakini wamekuwa wakilipa baadhi tu.
Mmoja wa wafugaji aliyefahamika kwa jina la Kuzenza Mtogambuli alisema yeye amechangia zaidi ya shlingi laki sita kwa ajili ya ununuzi wa mbao na mabati kwa madaasa mawili yanayotumiwa na wanafunzi wa shule hiyo.
Kwa upande wake Mwalimu Laiton Ngoli alisema kuwa mbali ya changamoto za madaasa shule hiyo haina nyumba ya mwalimu wala maliwato na kufanya baadhi ya watoto kujisaidi vichakani.
John Kalikumoyo aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Kijiji cha Ijumbi alisema kuwa shule hiyo ilipata kibali cha kujengwa mwaka 2013 lakini fedha zilizochangwa na wananchi hazionekani zilipo hali inayowakatisha tamaa wazazi.
Uchunguzi umebaini shule hiyo ina zaidi ya watoto 320 wanaosoma kwa kubadilishana madarasa hayo mawili na Mwalimu Ngoli anafundisha darasa la awali hadi darasa la sita ingawa watoto wa darasa la nne na darasa la sita wamesajiliwa shule ya msingi Ruiwa.
Kutoka shule hiyo ya Maendeleo Ishungu watoto hutembea umbali wa kilometa zaidi ya nane na hali inakuwa mbaya wakati wa masika ambapo watoto hushindwa kuhudhuria masomo kutokana na mto Gwili kujaa maji.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Maendeleo Charles Mkisi alisema kuwa wameanza kuchimba msingi  kutokana na fedha zilizochangwa lakini changamoto kubwa ni ukosefu wa ushikiano na Viongozi wa Kata ambapo wanakosa msaada wa usimamizi wa majengo hayo ambapo wameishia kuchimba msingi tu.
Kwa upande wake Afisa Elimu Mkoa wa Mbeya Regimius Ntimaya alisema kuwa atafuatillia suala hilo.

Na Ezekiel Kamanga 
Mbeya yetu

No comments:

Post a Comment