Tuesday, September 2, 2014

NDEGE YAANGUKA MBUGANI SERENGETI BAADA YA KUPOTEZA MAWASILIANO

Ndege 5Y SXP Fokker iliyoanguka Serengeti
NDEGE ya mizigo ya nchini Kenya iliyokuwa inatokea Mwanza kwenda Nairobi imeanguka baada ya kupoteza mawasiliano na mnara wa kuongozea (Control tower), na mabaki yake kuonekana katika eneo la
mbugani  Kongetende, Serengeti mkoani Mara.
Awali, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, (SACP), Valentino Mlowola, alithibitisha kutokea kwa tukio la kuanguka ndege hiyo yenye namba za usajili 5Y SXP Fokker 27  iliyoanza safari zake mjini Mwanza majira ya 1:26 usiku kwenda Nairobi.
Kwa mujibu wa taarifa ya awali kuhusu ajali hiyo iliyotolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga nchini (TCAA), Charles Chacha baada ya kutokea kwa ajali hiyo, mabaki ya ndege yameonekana katika eneo la Kogetende, asubuhi ya jana.
Hata hivyo, alisema kuwa hadi sasa hawana uhakika kama wafanyakazi waliyokuwema katika ndege hiyo wamepoteza maisha au laah.
Aliongeza kuwa, ndege hiyo ya mizigo inayomilikiwa na Kampuni ya Safari Express ya Nairobi Kenya, iliondoka uwanja wa ndege wa Mwanza saa 1: 26 usiku na ilitarajiwa kufika Nairobi saa  2:39 usiku kama isingepata ajali.
Chacha alieleza kuwa, mawasiliano ya mwisho na ndege hiyo yalikuwa saa 2:05 usiku wakati ndege ipo umbali wa kilometa 40 kutoka mpaka wa Tanzania na Kenya ikiwa angani futi 17,000 juu ya usawa wa bahari.
Alieleza ndege ilipaswa kuvuka eneo la mpaka wa Tanzania na Kenya saa 2:11 usiku, lakini ilipoteza mawasiliano na kituo kikuu cha kuongozea ndege cha Dar es Salaam na kwamba, hakukuwa na taarifa zozote kutoka kwa rubani wa ndege hiyo kuonyesha iwapo ilikuwa na tatizo au laah.
Alisema baada ya kubainika kwa mabaki hayo, mchakato wa uchunguzi wa ajali hiyo ili kubaini sababu iliyosababisha ajali hiyo umeanza na unawashirikisha wataalamu kutoka Mamlaka na Kitengo cha Uchunguzi wa Ajali.
 Via:Tanzania daima.

No comments:

Post a Comment