Sunday, April 27, 2014

WAJASILIAMALI WATAKIWA KUJIUNGA NA MIFUKO YA HIFADHI YA JAMII




Shinyanga.
ASILIMIA  kubwa ya wajasiliamali hapa nchini hawajajiunga na mifuko ya hifadhi ya jamii, hali inayofanya  kukosa  fedha za kuwasaidia katika maisha yao hasa pale wanapopatwa na matatizo kutokana na kuwa na kipato kidogo.

Hayo yalielezwa jana na mjumbe wa bodi ya mfuko wa  pensheni kwa watumishi wa umma(PSPF )kutoka jijini Dar es salaam Clement  Mswanyama, alipokuwa akitoa elimu kwa  wajasiliamali wa soko kuu la mjini Shinyanga  juu ya umuhimu wa kujiunga na mifuko hiyo na kuwataka  kuchukuwa hatua ili kufanya  mabadiliko katika familia zao sanjari na kujiwekea akiba ya uzeeni.

Mswanyama alibainisha kuwa  watu wanaofanya shughuli zenye kipato kidogo  wamekuwa wakisahaulika kupewa fursa ya kujiunga na mifuko hiyo ,kwa kuwathamini watumishi ambao wameajiriwa hivyo  huwajengea watu hao mazingira ya kuwa na maisha magumu.

“Mfuko wa hifadhi ya jamii utakusaidia  kujiwekea hazina ya fedha ambazo zitaboresha maisha yako  hasa pale anapopatwa na matatizo ya kifamilia ,pia manufaa mengine ya kujiunga ni kupata mafao  ya uzeeni na  kuendelea kuwa na maisha mazuri” alisema Mswanyama.

Alisema hapo awali shirika hilo la PSPF lilikuwa linahudumia  watumishi wa serikali pekee, lakini kutokana na kuona idadi kubwa ya wafanyabishara wa kujitegemea kusahaulika  katika mpango huo na kunyimwa fursa,  ndipo waliamua kupanua wigo na kuwapa nafasi wajasiliamali kuchangia fedha kidogo shilingi Elfu kumi kwa kila mwezi .

Kwa upande wake  meneja wa Shirika hilo mkoani Shinyanga Erick Chanimbaga, alisema wameamua kutoa elimu kwa wajasiliamali wote wa mkoa huo  kwa kushirikisha wafanyabishara wa masoko, mama Lishe,waendesha bodaboda, wafanyakazi wa viwandani ili kuwajengea msingi mzuri wa maisha kutokana na utunzaji wa fedha katika mifuko ya hifadhi ya jamii.

Nao baadhi ya wajasiliamali  wa soko hilo  Rehema  Pius na Daniphod  Mshumbusi,walisema elimu waliyoipata itawasaidia kufanya maamuzi mazuri ya kuchagua mifuko ya hifadhi ya jamii ya kujiunga nayo ili kujiwekea akiba ya uzeeni pia kusaidia familia wakati wa shida kwa kuwa kipato chao ni kidogo.

“Leo nimepata uelewa zaidi juu ya mifuko hii ya jamii siku zote nilikuwa najiuliza maswali mengi lakini sipati majibu,sasa kupitia elimu hii iliyotolewa na PSPF nimeelewa ,licha ya vipato vyetu ni vidogo sisi wajasiliamali kumbe tunaweza tu kujiunga  na kulipia kiasi kidogo kila mwezi”alisema Rehema.

No comments:

Post a Comment