Tuesday, June 24, 2014

FISI AZUA BALAA GEITA AJERUHI WATU KWA KUWA UMA MIGUU NA MIDOMO WANANCHI WAGOMBANIA NYAMA YAKE BAADA YA KUUAWA, BONYEZA HAPA UPATE TUKIO ZIMA.





 FISI ALIYESHAMBULIA WATU KWA KUWAUMA MIGUU NA MIDOMO ,WANANCHI WAGOMBANIA NYAMA YAKE  BAADA YA KUUAWA NA KUFANYA KUWA KITOWEO.

MATUKIO yanayohusishwa na imani za kishirikina ya watu kushambuliwa na Fisi hususani watoto chini ya Umri wa miaka Mitano sasa yamechukua sura mpya mkoani Geita baada ya fisi mwingine kuvamia mtaa na kuanza kushambulia watu hovyo kwa kuwauma kabla ya polisi kufika eneo hilo na kumuua kwa risasi kisha kutoa mwanya kwa wananchi kugombea nyama yake na kuifanya kitoweo.
Tukio hilo la kusitaajabisha na ambalo limeacha maswali mengi,limetokea jana,majira ya saa 9 alasiri katika mtaa wa Kabahelele,Kata ya Katoro Wilaya ya Geita Mkoani Geita.
Mashuhuda wa tukio hilo waliuambia mtandao  wa malunde1 blog kuwa,mara baada ya fisi huyo mkubwa mithiri ya Ndama kuvamia kwenye mtaa huo wananchi walishikwa na taharuki wasijue la kufanya.
Walidai kuwa,wakiwa wanajiandaa kuchukua hatua dhidi ya Fisi huyo,walishangaa kuona akivamia watu mmoja baada ya mwingine na kuanza kuwauma na ndipo walipopiga kelele kisha kukusanyika na kumweka kati mnyama huyo huku wengine wakipiga simu polisi kuomba msaada.
Wakati polisi wanafika eneo hilo,tayari Fisi huyo alikuwa amekwishafanya madhara kwa watu watatu ambao waling’atwa sehemu za miguuni na midomoni hali iliyowalazimu polisi kutawanya watu kisha walifanikiwa kumuua fisi huyo kwa kumpiga risasi zaidi ya mbili.
Waliojeruhiwa na Fisi katika tukio hilo,ni pamoja na Bugamba Zumbe(21),Peter Francis (32),na mwingine ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja wote wakazi wa mtaa huo wa Kabahelele.
Hata hivyo katika hali ya kushangaza baada ya Fisi huyo kuuawa,baadhi ya wananchi wa eneo hilo nusura wauane kwa kukatana visu wakigombea nyama ya mnyama huyo na walipohojiwa sababu za kugombea nyama hiyo walidai inaliwa na kwamba ikipikwa vizuri inazidi hata ile ya ng’ombe.
‘’Ndugu mwandishi huyu mnyama pamoja na kwamba ni mchafu lakini nyama yake ikipikwa kwa kuandaliwa vyema ni nzuri kuliko hata ile ya ng’ombe ndiyo maana unaona watu wanataka kukatana visu lengo kila mmoja apate hata kipande kimoja maisha yenyewe magumu hapa tumeokoa pesa ya mboga’’alisema mwanamke aliyefahamika kwa jina moja la Helena mkazi wa Mtaa huo.
Ofisa Maliasili wa Wilaya ya Geita Kasika Gamba alidai kuwa,chanzo cha Fisi kushambulia watu,ni kutokana na uharibifu wa mazingira katika Hifadhi za Mistu hali ambayo imesababisha wanyama hao kuzagaa kwenye makazi ya watu kutokana na kukosa sehemu ya kijihifadhi na kujipatia chakula.

Kwa upande wake Daktari wa Mifugo wa Wilaya ya Geita Thobias Kiputa,aliwataka wananchi kuepuka kula hovyo nyama za wanyama ambao siyo wanyama(Meat Animals)ambao ni wala nyama kama Fisi ambao hawajakaguliwa wanaoweza kuwa na magonjwa mbalimbali yanayoweza kuwasababishia madhara ya afya na badala yake wajitahidi kula nyama itokanayo na wanyama wa nyama katika maeneo yao ambao mara nyingi wanakuwa wamekaguliwa na wataalamu wa mifugo.
‘’Haipendezi watu kula nyama ya wanyama wala nyama(Meat Animals),kwani wanaweza kuwa na magonjwa mbalimbali maana fisi ni wanyama wala nyama na wanaweza kuwa na magonjwa mbalimbali,watu wasipende kula wanyama hao kwa kuwa wanakuwa hawajakaguliwa na si utamaduni wetu’’
‘’Na si desturi wataalam kukagua wanyama wa aina hiyo ninachowashauri wananchi wajitahidi kula nyama itokanayo na wanyama wa nyama kwenye maeneo yao, ambao mara nyingi wanakuwa wamekaguliwa na wataalamu wa mifugo’’kwani  wanaweza kula nyama ya aina hiyo(Fisi) wakapata madhara ya kiafya’’alisema Dakta Kiputa.

Mwishoni mwa wiki iliyopita Mwanaume mmoja mwenye Umri wa miaka 35 mkazi wa Nyabulanda Tarafa ya Nyang’hwale Wilayani Nyang’hwale Mkoani Geita aliuawa kwa kushambuliwa na Fisi na kuliwa,sehemu za Tumbo,mguu mmoja ukiwa umebaki mfupa na ule wa kulia haupo pamoja sehemu za usoni kichwani na kifuani.

Matukio ya fisi kushambulia na kula watu yamekuwa yakitokea mara kwa mara mkoani Geita hasa kwenye Halmashauri za wilaya za Nyang'hwale na Geita ambapo mara nyingi kundi linaloadhirika zaidi na wanyama hao ni watoto wenye umri chini  miaka 5.

Chanzo. Na Victor Bariety  -Malunde1 blog Geita.
 

No comments:

Post a Comment